Thursday, 2 October 2014

Kura za Z’bar ni pasua kichwa


Mwenyekiti wa Bunge la katiba Samweli Sitta akizungumza Bungeni Dodoma jana.PICHA|MAKTABA 
Na Mwandishi Wetu, Mwananchi
Ili kupata theluthi mbili, zinatakiwa kura 146, idadi ambayo kutimia kwake kwa mujibu wa takwimu zilizopo hadi sasa zinatakiwa kura nyingine za ‘ndiyo’ 14.

Dar es Salaam. Suala la akidi ya wajumbe wa Bunge Maalumu kutoka Zanzibar linazidi kusumbua vichwa vya uongozi wa Bunge hilo kiasi cha kusababisha wasiwasi mkubwa kuhusu hatima ya Rasimu ya Katiba inayopendekezwa.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa hadi jana, ni wajumbe 143 tu kati ya 219 kutoka upande huo waliokuwa wamepiga kura, huku wajumbe 86 wakiwa bado hawajatimiza haki yao hiyo ya kidemokrasia.
Kati ya wasiopiga kura, 66 ni wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao walisusia Bunge hilo Aprili 16, mwaka huu kutokana na kile walichodai kuwa ni kutoridhishwa na jinsi Bunge linavyoendeshwa, wakati wajumbe 20 hawajapiga kura kutokana na sababu mbalimbali zikiwamo za kwenda kuhiji Saudi Arabia.
Jana asubuhi, Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta alisema licha ya njama zinazofanywa na watu kukwamisha rasimu hiyo isipate kura za kutosha, mipango yao haitafanikiwa kwani kulikuwa na kila dalili kwamba kazi hiyo ingehitimishwa kwa ufanisi.
Hata hivyo, uchambuzi wa kitakwimu unaonyesha kuwa kulikuwa na kila dalili ya kukosekana kwa theluthi mbili ya kura zinazotakiwa kwa mujibu wa sheria kwa upande wa Zanzibar kwani kati ya 143 ya waliopiga kura, saba kati yao walipiga kura ya ‘hapana.’
Kadhalika, wajumbe wawili akiwamo Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Othman Masoud Othman walipiga kura wakikataa baadhi ya ibara, wakati kura za ‘ndiyo’ zilikuwa 105.
Kitendawili kinachosubiriwa kilikuwa ni kuhusu kura 30 za siri ambazo hadi jana matokeo yake yalikuwa hayajawekwa wazi, huku kukiwa hakuna taarifa zozote kuhusu kura zilizotarajiwa kupigwa na wajumbe 20 ambao hawapo Dodoma.
Awali, kulikuwa na mpango wa kuwawezesha wajumbe hao kupiga kura huko waliko na uongozi wa Bunge Maalumu ulikusudia kupeleka ofisa wake, Makka, Saudi Arabia ili kuwawezesha wajumbe wake wanane ambao ni mahujaji kupiga kura wakiwa huko.
Ili kupata theluthi mbili, zinatakiwa kura 146, idadi ambayo kutimia kwake kwa mujibu wa takwimu zilizopo hadi sasa zinatakiwa kura nyingine za ‘ndiyo’ 14.
Kwa maana hiyo hata kama kura zote za siri 30 zitaunga mkono rasimu hiyo, bado haziwezi kuiwezesha kupata kura zinazotakiwa kwani zitafikia 135, hivyo kuendelea kuwapo pengo la kura 9 ili kufikisha kura 146.
Msako wa kura
Kutokana na mazingira hayo, habari zilizolifikia gazeti hili juzi na jana zinasema kulikuwa na jitihada kubwa za kuwashawishi baadhi ya wabunge wa Ukawa wapige kura.

No comments:

Post a Comment