Thursday, 2 October 2014

Mwanasheria Mkuu Z’bar azikataa ibara 22 Katiba


Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Othman Masoud Othman.
“Kwa hiyo kama Serikali haikuwa na msimamo kwa maana ya upande, maana yake ni ipi pengine unisadie… nilipiga kura kwa kuzingatia utashi wangu na maoni yangu.”

Dodoma.Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), Othman Masoud Othman amezua kizaazaa bungeni baada ya jana kupiga kura ya ‘hapana’ katika ibara 22 kwenye Rasimu ya Katiba iliyopendekezwa.
Akipiga kura hiyo, Othman ambaye hivi karibuni alijiondoa katika Kamati ya Uandishi kwa kutoridhika na baadhi ya mambo, alieleza kutokubaliana na ibara ya pili, tisa, 86, 37, 70 hadi 75 na Sura ya 11 ambayo ina ibara ya 158, 159, 160 na 161 pamoja na Sura ya 16 yenye ibara za 243 hadi 251 na Nyongeza ya Kwanza inayozungumzia mambo ya Muungano.
Hatua hiyo ilionekana kuwaudhi baadhi ya wajumbe kiasi cha kumzomea, hivyo baada ya Bunge kuahirishwa alilazimika kutolewa mlango wa nyuma wa Ukumbi wa Bunge ambao hutumiwa na Waziri Mkuu huku akiwa amesindikizwa na wanausalama kwa kuhofia vurugu.
Wakati akisindikizwa, alikuwa ameongozana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud na Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho.
Kwanza alipelekwa kwenye chumba kimojawapo katika jengo la Bunge ambako alikaa kwa nusu saa kabla ya kutolewa nje ya eneo la Bunge ambako alipanda gari alilokuwamo Kificho na kuondoka.
Hatua hiyo ya Othman imekuja wakati Waziri wa Sheria wa Zanzibar, Abubakary Khamis Bakary (CUF) akiwa hayumo bungeni baada ya kususia vikao hivyo pamoja na wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Watanzania (Ukawa).
Baadaye Othman aliliambia gazeti hili kwamba licha ya kuwa yeye ni Mwanasheria Mkuu wa SMZ alitumia utashi wake wa kidemokrasia kupiga kura kuzikataa ibara hizo, kutokana na kutoridhishwa na jinsi zilivyoandikwa.
“Katika suala la Katiba, Serikali ilishatamka kwenye Baraza la Wawakilishi na hata nje ya Baraza kwamba haina msimamo. Ndiyo maana uliona misimamo ilikuwa imeachwa kwenye vyama vya siasa, sasa mimi siyo Mwanasheria Mkuu wa chama chochote.
“Kwa hiyo kama Serikali haikuwa na msimamo kwa maana ya upande, maana yake ni ipi pengine unisadie… nilipiga kura kwa kuzingatia utashi wangu na maoni yangu.”
Alisema awali, alikuwa ameamua kutopiga kura lakini baadhi ya watu wenye busara walimshauri kutumia demokrasia yake kuonyesha yale anayokubaliana nayo na yale asiyoyakubali… “Mtu unaweza kuwa na msimamo fulani, lakini kwa jinsi binadamu tulivyo, siyo lazima msimamo wako uwe sahihi, kwa hivyo na mimi niliwasikiliza watu wenye busara nikaona ushauri wao unafaa ndiyo maana nilikwenda kupiga kura.”
Ashambuliwa bungeni
Baada ya Othman kupiga kura hiyo, Mbunge wa Chwaka, Yahya Kassimu Issa, aliomba mwongozo wa mwenyekiti na kumshambulia kwa hatua hiyo.

No comments:

Post a Comment